Saturday, June 8, 2013

Kunauwezekano wa kugawanywa ikulu ya rais:Warioba

Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini Tanzania, Jaji Joseph Warioba amesema iwapo Mfumo wa Serikali Tatu utaridhiwa na wananchi ni lazima mambo yaliyo ndani ya Muungano yatagawanywa ikiwa ni pamoja na Ikulu ya Rais. Amesema kutokana na taifa kufanya mabadiliko ya Katiba ni lazima kuwepo mpangilio wa kugawana mambo mbalimbali yaliyokuwa chini ya Muungano ikiwamo majengo, wafanyakazi, Ikulu, hata vitendea kazi na kwamba utaratibu huo ni kama ule uliotumika wakati Tanganyika na Zanzibar zilipoungana. Kauli ya hiyo ya Jaji Warioba imekuja siku tatu tangu Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe kueleza kuwa Tanzania Bara itaanza mchakato wa kutunga Katiba yake Aprili mwaka 2014 na kumalizika Desemba mwaka huohuo. Jaji Warioba aliyasema hayo katika mahojiano maalumu na waandishi wandamizi wa habari jijini Dar es salamu, Tanzania. Hata hivyo aliongeza kuwa suala hilo linahitajia mazungumzo ya pande zote mbili, baada ya kukamilika kwa mchakato huu kwa sababu hii ni rasimu tu, ambayo itajadiliwa na wananchi kabla ya kuanza kwa Bunge la Katiba na baadaye kuwepo kwa kura ya maoni.

No comments:

Post a Comment